emblem

The United Republic of Tanzania

National Social Security Fund (NSSF)

We Build Your Future

News

NSSF YATOA ELIMU YA HIFADHI YA JAMII KATIKA MKUTANO MKUU WA SABA WA JUKWAA LA WAHARIRI





Na MWANDISHI WETU, LINDI



Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), umeshiriki na kutoa elimu ya hifadhi ya jamii katika Mkutano Mkuu wa Saba wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) uliofanyika Mkoani Lindi.



Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Robert Kadege Meneja wa Huduma kwa Wateja, alisema miongoni mwa elimu iliyotolewa ni pamoja na elimu kuhusu majukumu ya waajiri, faida na mafao ya wanachama, pamoja na elimu ihusianayo na kazi za Mfuko kwa ujumla.



Bw. Kadege ambaye ni Meneja wa Huduma na Wateja alisema Mfuko unaendelea kuwakumbusha waajiri wote wa sekta binafsi kuwasilisha michango yao pamoja na ya wanachama wao kwa wakati kwani ni takwa la sheria.



Alisema katika kuhakikisha waajiri wanalipa michango kwa wakati, Mfuko umeweka mifumo mbalimbali ukiwemo wa Employer Portal ambapo mfumo huo unamuwezesha mwajiri kuwasilisha michango popote alipo bila ya kulazimika kufika ofisini.



Naye, Meneja Uhusiano na Elimu kwa Umma wa NSSF, Bi. Lulu Mengele, alisema kwa kutambua umuhimu wa vyombo vya habari Mfuko ulionelea ni vyema ushiriki katika mkutano huo kwa lengo la kutoa elimu ya hifadhi ya jamii kwa wahariri ambao ni wadau muhimu.



“Kama tunavyojua mwaka 2018, Serikali ilifanya maboresho makubwa katika sekta ya hifadhi ya jamii yaliyopelekea NSSF kuwa Mfuko pekee unaohudumia wanachama kutoka sekta binafsi na sekta isiyo rasmi, kwa hiyo NSSF tumeona hii ni fursa ambayo tumeipata kupitia jukwaa la wahariri. Bi. Lulu aliendelea kwa kusema vyombo vya habari ni daraja la moja kwa moja kati ya Mfuko na wanachama wakiwemo wananchi.



"Tunatambua mchango mkubwa wa wahariri na vyombo vya habari kwa ujumla katika kupeleka taarifa sahihi kwa jamii, wahariri wakipatiwa taarifa sahihi na wao wataweza kuhabarisha kwa usahihi zaidi", alisema Bi. Lulu.




NSSF ilitumia fursa hiyo kuwakaribisha wananchi ambao hawajajiunga na Mfuko kutembelea ofisi mbalimbali za NSSF ili waweze kujiunga na kuanza kuchangia kwa ajili ya kujiwekea akiba zao



Kwa upande wake, Meneja wa NSSF Mkoa wa Lindi, Juma Namuna, amesema Mfuko katika Mkoa huo unaendelea kutekeleza majukumu yake ya msingi ambayo ni kutoa elimu na kuandikisha wanachama wapya, kukusanya michango na kulipa kwa wakati.