emblem

The United Republic of Tanzania

National Social Security Fund (NSSF)

We Build Your Future

News

NSSF YAZIDI KURAHISISHA UPATIKANAJI WA HUDUMA ZAKE KIDIJITALI





*Ni kupitia mfumo wa NSSF Taarifa mwanachama anaweza kupata taarifa zake kiganjani popote alipo



Na MWANDISHI WETU,
Tanga. Mfuko wa Taifa wa Hifadhi za Jamii (NSSF), ulishiriki katika Maonesho ya 11 ya Biashara na Utalii yaliyofanyika kwenye Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara Jijini Tanga, na kutumia fursa hiyo kutoa elimu na huduma mbalimbali za hifadhi ya jamii huku ukiwataka wanachama wake kutumia huduma ya NSSF Taarifa ili kupata taarifa zao mbalimbali kiganjani zikiwemo za michango popote walipo bila ya kulazimika kufika ofisi za NSSF.



Hayo yamesemwa na Afisa Matekelezo Mkuu wa NSSF Mkoa wa Tanga, Bw.Abubakari Mshangama. Amesema NSSF Taarifa ni mfumo rafiki na rahisi unaowawezesha wanachama kupata taarifa binafsi, michango na madai yao.



Bw. Mshangama amesema huduma hiyo inapatikana kupitia simu ya kiganjani kwa njia tatu ambazo ni ujumbe mfupi (SMS), programu ya simu ya kiganjani (Mobile App) ya NSSF na WhatApp.



“Tupo hapa kwenye maonesho haya kimkakati kwa kutoa elimu kuhusu huduma zetu mbalimbali, pia kuitangaza programu hii ya kidijitali zaidi ambayo inamuwezesha mwanachama kupata taarifa na huduma kwa njia ya ujumbe mfupi,” amesema Bw. Mshangama.



Aidha, amesema kupitia maonesho hayo NSSF inaendelea kutoa elimu ya hifadhi ya jamii hususan katika kutekeleza majukumu yake ya msingi ambayo ni kuandikisha wanachama, kukusanya michango, kutangaza fursa za uwekezaji za nyumba, viwanja pamoja na elimu kuhusu mafao.



Awali, akizungumza mara baada ya kutembelea banda la NSSF, Mkuu wa Wilaya ya Muheza, Mhe. Zainab Abdallah amewataka wafanya kazi waliopo katika sekta rasmi na wajasiriamali kujiunga na NSSF ili kunufaika na mafao mbalimbali yanayotolewa.



“Niendelee kuwahimiza wafanyakazi na waajiri wajue kwamba ni takwa la kisheria wahakikishe wanawasajili wafanyakazi NSSF ili kuweza kunufaika na mafao mbalimbali,” amesema.